Na: Nassoro Rashid – Mkinga
Wananchi wa Kijiji cha Kisiwani 'A', Kata ya Daluni wilayani Mkinga wamehimizwa kuupokea, kuumiliki na kuusimamia vyema Mradi wa Mageuzi ya Tasnia ya Maziwa na Mabadiliko ya Tabianchi ili kufikia malengo yaliyokusudiwa ya kuboresha maisha na kipato cha wafugaji.
Wito huo umetolewa na Afisa Mifugo wa Wilaya ya Mkinga, Ndugu Hosea Noel, wakati akiutambulisha mradi huo mbele ya wananchi wa kijiji hicho, akieleza kuwa Halmashauri ya Wilaya ya Mkinga imebahatika kuwa miongoni mwa halmashauri 21 pekee nchini zilizochaguliwa kunufaika na mradi huo kati ya halmashauri 184 zilizopo Tanzania Bara na Visiwani.
Amesema mradi huo uko chini ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi kwa kushirikiana na wahisani mbalimbali, akilitaja Shirika la IFAD kuwa mhisani mkubwa, na kwamba utekelezaji wake utachukua muda wa miaka 10.
“Mradi huu unalenga kuleta mageuzi makubwa kwenye sekta ya maziwa kuanzia uzalishaji, huduma za ugani hadi masoko na uchakataji wa maziwa, ili mfugaji aweze kunufaika moja kwa moja,” amesema Noel.
Amefafanua kuwa katika upande wa uzalishaji, mradi utahusisha ugawaji wa ng’ombe wa maziwa, mafunzo ya ufugaji bora, huduma za upandikizaji kwa chupa, upandaji na uhifadhi wa malisho kwa lengo la kuongeza uzalishaji wa maziwa na kupata ng’ombe bora wenye tija.
Kwa mujibu wa Afisa huyo, asilimia 20 ya wanufaika wa mradi italenga kaya zenye uhitaji mkubwa, ambapo watapatiwa ng’ombe mmoja wa maziwa bure pamoja na ujenzi wa banda na huduma nyingine muhimu.
“Lengo ni kumkwamua mwananchi aliyekuwa katika hali duni kabisa aweze kuinuka kiuchumi na angalau awe na uhakika wa chakula na kipato,” amesisitiza.
Ameonya kuwa uchaguzi wa wanufaika hao lazima ufanyike kwa uadilifu mkubwa kupitia Serikali ya Kijiji na Halmashauri, akibainisha kuwa dosari yoyote inaweza kusababisha mradi huo kuondolewa na kupelekwa eneo jingine.
Kwa upande wa asilimia 80 ya wafugaji waliobaki, amesema watanufaika kwa kuchangia asilimia 25 ya gharama ya ng’ombe kupitia utaratibu wa mkopo utakaowekwa wazi, huku akieleza kuwa mfumo wa “ndama wa kwanza jike kumpa mwingine” utatumika ili kuongeza idadi ya wanufaika katika jamii.
Aidha, amesema mradi utahakikisha upatikanaji wa huduma za uhakika za upandikizaji kwa chupa kwa kuwapatia vifaa wapandishaji wa wilaya, hatua itakayosaidia kupunguza matumizi ya madume duni na kuongeza uzalishaji wa maziwa bora.
Katika upande wa masoko, Noel amesema wahusika wa masoko watahusishwa kutafuta masoko ya uhakika kwa wafugaji, na pale itakapobainika hakuna soko la moja kwa moja, wafugaji watafundishwa uchakataji wa maziwa kuwa bidhaa mbalimbali kama maziwa ya mgando.
Akihitimisha, Afisa Mifugo huyo amewataka wananchi kushiriki kikamilifu katika utekelezaji wa mradi huo, akisisitiza kuwa miradi ya serikali hutathminiwa kwa matokeo, na endapo juhudi hazitaonekana, huondolewa.
“Mradi huu ni fursa adhimu kwa Wilaya ya Mkinga, tuupokee, tuulinde na tuhakikishe tunafikia malengo yake,” amesema.

Kasera, Tanga -HorohoroRoad
Postal Address: P O Box 6005 Tanga
Simu: +255 027-2660501
Simu: +255 684 625 299
Barua Pepe: Info@mkingadc.go.tz
Mkinga dc @ 2017