Na: Nassoro Rashid
Serikali kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo inaendelea kutekeleza Mradi wa Mageuzi ya Tasnia ya Maziwa na Mabadiliko ya Tabianchi, unaolenga kuboresha uzalishaji wa maziwa na kuongeza kipato cha wananchi.
Akizungumza katika mahojiano, Mtaalamu wa masuala ya jamii kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Ndugu Charles Lugamala, amesema mradi huo unatekelezwa kwa ushirikiano kati ya Serikali na wadau wa maendeleo wakiongozwa na Mfuko wa Kimataifa wa Maendeleo ya Kilimo (IFAD), ukiwa ni mradi wa kimkakati wa kuleta mageuzi ya kweli katika sekta ya mifugo nchini.
“Huu ni mradi wa kimkakati wa Serikali unaolenga kuleta mageuzi makubwa katika tasnia ya maziwa nchini kwa kuzingatia uzalishaji wenye tija, uwezo wa kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi na kuongeza kipato cha wananchi,” amesema Lugamala.
Ameeleza kuwa mradi huo wa miaka 10 unatekelezwa katika mikoa 8 ya Tanzania Bara, ikiwemo Tanga, na kwa Mkoa wa Tanga unahusisha Halmashauri za Mkinga, Lushoto na Muheza. Mradi unatarajiwa kunufaisha jumla ya kaya 140,000, sawa na wanufaika wapatao 700,000 moja kwa moja.
Kwa mwaka wa kwanza wa utekelezaji, kaya 29,000 zinatarajiwa kuanza kunufaika, huku Halmashauri ya Wilaya ya Mkinga ikitarajiwa kuwa na wanufaika wasiopungua 718.
Amefafanua kuwa mradi unatoa fursa katika maeneo makuu matatu ambayo ni uzalishaji, masoko na uratibu wa mradi. Katika uzalishaji, mradi unalenga kuboresha mbegu bora za mifugo, malisho, huduma za maji na tiba ya mifugo ili kuongeza tija ya uzalishaji wa maziwa.
Kwa upande wa masoko, mradi utaimarisha mnyororo wa thamani wa maziwa kuanzia ukusanyaji, usindikaji hadi miundombinu ya usafirishaji, ikiwemo ukarabati wa barabara zenye urefu wa kilometa 173 katika maeneo ya mradi.
Aidha, mradi utatoa fursa za kifedha ikiwemo mikopo yenye riba nafuu na kuimarisha ujasiriamali kwa wadau wa tasnia ya maziwa ili kuongeza uzalishaji na kipato cha wananchi.
Katika vipaumbele vya wanufaika, Lugamala amesema mradi umezingatia makundi yaliyoachwa nyuma kwa muda mrefu, hususan wanawake, vijana na watu wenye ulemavu, ili kuhakikisha wanashiriki kikamilifu katika fursa za kiuchumi zinazotokana na tasnia ya maziwa.
Kuhusu tukio la Mkinga, amesema uwepo wao ni kwa ajili ya kuzindua Jukwaa la Wadau wa Maziwa, linalowakutanisha wazalishaji, wasindikaji, taasisi za fedha, vyama vya ushirika na wadau wengine kwa lengo la kujadili fursa, changamoto na kuweka vipaumbele vya maendeleo ya tasnia ya maziwa kwa manufaa ya wananchi.

Kasera, Tanga -HorohoroRoad
Postal Address: P O Box 6005 Tanga
Simu: +255 027-2660501
Simu: +255 684 625 299
Barua Pepe: Info@mkingadc.go.tz
Mkinga dc @ 2017