Na: Dominick Cosmas - Mkinga
Mbunge wa Jimbo la Mkinga, Mhe. Twaha Said Mwakioja, amewataka wanufaika wa mikopo ya asilimia 10 inayotolewa na Halmashauri ya Wilaya ya Mkinga kuitumia mikopo hiyo kwa malengo yaliyokusudiwa ili kujiajiri, kuongeza kipato na kuchangia kupunguza umaskini katika jamii.
Mhe. Mwakioja ameyasema hayo Desemba 23, 2025, wakati akizungumza na wanufaika wa mikopo hiyo katika ukumbi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mkinga, akieleza kuwa kurejea kwa mikopo hiyo ni faraja kubwa kwa wananchi wa Mkinga baada ya kusimama kwa muda mwaka 2023 ili kuweka mifumo bora ya uwazi na ufanisi.
“Ni wajibu wetu sisi wana Mkinga kumshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kurejesha mikopo hii ambayo sasa inalenga kuwafikia wananchi kwa uwazi na kuleta tija halisi,” alisema Mbunge huyo.
Alieleza kuwa tangu kurejeshwa kwa mikopo hiyo mwaka 2024 na kuendelea mwaka 2025, zaidi ya shilingi milioni 546 zimetolewa kwa wananchi wa Mkinga pekee, fedha ambazo zimelenga makundi mbalimbali ya kijamii.
Kwa mujibu wa Mbunge huyo, katika kipindi cha mwaka mmoja na nusu, vikundi 54 vya wanawake vimenufaika na mikopo yenye jumla ya zaidi ya shilingi milioni 290, huku vijana nao wakinufaika na zaidi ya shilingi milioni 247, akisisitiza kuwa mikopo hiyo haina riba na inalenga kuwawezesha wananchi kiuchumi.
Mbunge huyo alibainisha kuwa serikali haitoi mikopo hiyo kama sadaka bali kama chombo cha utekelezaji wa malengo makuu matatu; kwanza kuwawezesha wananchi kujiajiri na kuanzisha biashara zitakazozalisha ajira kwao na kwa wengine, pili kuongeza uzalishaji wa kipato ili kupunguza umaskini, na tatu kuwajengea wananchi utamaduni wa kushirikiana kupitia vikundi.
Ameupongeza uongozi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mkinga wakiwemo Mwenyekiti wa Halmashauri, Mkurugenzi Mtendaji, Wakuu wa Idara pamoja na watumishi wote wanaosimamia zoezi la utoaji na ufuatiliaji wa mikopo hiyo, kwa kuhakikisha fedha hizo zinawafikia walengwa.

Kasera, Tanga -HorohoroRoad
Postal Address: P O Box 6005 Tanga
Simu: +255 027-2660501
Simu: +255 684 625 299
Barua Pepe: Info@mkingadc.go.tz
Mkinga dc @ 2017